
Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) Mkoa wa Kagera imewafikisha Mahakamani wafanyabiashara watano na kuwafungulia mashtaka tisa ya uhujumu uchumi ikiwemo kukwepa kulipa kodi zaidi ya shilingi milioni kumi na kutengeneza pombe kali bila kuwa na leseni.
Washtakiwa hao wamefikishwa katika mahakama ya Hakimu Mkazi Mfawidhi wa mahakama ya Bukoba, Janeth Masesa na kusomewa mashtaka yanayowakabili ambayo waliyatenda kati ya Desemba 2024 na Februari 2025.

Advertisement
Kesi ya kwanza namba 7238 ya mwaka 2025 inawakabili washtakiwa wanne ambao ni Mwesiga Reopard, Nelius Kaizilege, Julieth Ishengoma na Herieth Gervas walioisababishia TRA hasara ya zaidi ya shilingi milioni kumi,
Kesi ya pili namba 7243 ya mwaka 2025 ni ya mshtakiwa Mulokozi Egbert (39) anayekabiliwa na mashtaka nane ambapo aliisababishia hasara TRA zaidi ya shilingi milioni moja.

Mashtaka mengine yanayowakabili ni pamoja na kushindwa kuomba kibali cha kutengeneza bidhaa zenye ushuru kwa ajili ya eneo la utengenezaji na utunzaji, kushindwa kuwasilisha marejeo ya bidhaa zenye ushuru zilizozalishwa, kushindwa kutunza kumbukumbu za stempu za kielektroniki na kusaidia ukwepaji kodi ya ushuru wa bidhaa.
Hata hivyo washtakiwa wote wamekana mashtaka hayo na kupata dhamana baada ya kutimiza vigezo.

Kwa upande wa Jamhuri kesi hiyo inasimamiwa na mawakili wa serikali ambao ni Judith Mwakyusa, Grolia Lugeye na Alex Giryago huku kwa upande wa utetezi ni wakili Projestus Mulokozi na Frank Kaloli.
Kesi ya kwanza inayowakabili washtakiwa wanne itaendelea tena Aprili 8 huku kesi ya pili itaendelea tena Aprili 2 mwaka huu.